WIZARA ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, imesema kuwa 
umasikini uliokithiri miongoni mwa jamii ni moja ya chanzo cha wimbi 
kubwa la watoto wa mitaani.
  Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Vijana, Elisante ole Gabriel, 
alitoa kauli hiyo juzi wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika 
iliyoandaliwa na Shirika la Hope for the Children Organization.
Akizungumza kwa niaba yake, ofisa mwandamizi wa idara hiyo, Focas 
Kapinga, alisema jamii inapaswa kutambua kuwa jukumu la kuwalea watoto 
hao ni la Watanzania wote.
  Kwamba umasikini umekuwa ukichangia hali hiyo ya watoto wa mitaani 
kutokana na baadhi ya wazazi kushindwa kuzihudumia familia zao ipasavyo,
 matokeo yake watoto huamua kukimbilia mitaani kwa matumaini ya kupata 
maisha bora.
Kapinga alisema kuvunjika kwa ndoa kumekuwa kukisababisha familia 
kushindwa kukidhi mahitaji muhimu kwa watoto, kama vile elimu, chakula, 
mavazi hali inayowalazimisha kuondoka majumbani kwao.
  Alibainisha kuwa, wizara hiyo ndiyo yenye jukumu la maendeleo ya 
vijana, wakiwemo watoto, na kwamba dhamira yao ni kukabiliana na mambo 
yanayosababisha watoto kukimbilia mitaani.
  “Wizara imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali yakiwemo mashirika 
ya kimataifa kama vile UNICEF, ILO, UNEPA, UNDP na ya watu binafsi 
yaliyoko nchini na taasisi za dini katika kutimiza azma yake,” alisema.
  Kapinga alibainisha kuwa, jitihada hizo ni pamoja na utoaji wa elimu 
ya ujasiriamali, stadi za maisha na mikopo kwa vijana yenye masharti 
nafuu.
  Awali Mkurugenzi wa Hope for the Children Organization, Joyce Mang’o, 
alisema pamoja na mipango mingi ya serikali, lakini bado imekuwa ikitoa 
mchango hafifu wa kupambana na tatizo hilo.
  Alisema sheria zilizopo hazilengi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa 
asasi na watoto pia, jambo linalosababisha asasi kuwa na utendaji hafifu
 usiokidhi haja na matakwa kwa wahusika.
No comments:
Post a Comment