WATU tisa wamefariki papo hapo na wengine 20 kujeruhiwa katika 
ajali iliyohusisha magari mawili eneo la Ntangano Ijombe Mbeya Vijijini 
barabara ya Mbeya- Kyela.
Ajali hiyo imelihusisha roli lenye namba za usajili T.658 ASJ 
lililokuwa na tela namba T.150 ASN iliyokuwa ikitokea mpakani mwa 
Tanzania na Malawi (Kasumulu) pamoja na Costa yenye namba T.886 BDZ 
iliyokuwa ikitokea jijini Mbeya kuelekea wilayani Kyela.
  Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Mbeya Dk. Eliuter Samky amethibitisha
 kupokea maiti tisa wakiwamo wanawake watatu pamoja na majeruhi 20 na 
kusema kuwa mara baada ya majeruhi kufikishwa hospitalini hapo watu 
wanne walipoteza maisha wakiwa katika harakati za kupatiwa matibabu.
“Ni kweli tumepokea idadi hiyo ya maiti lakini kati ya majeruhi 20 
tuliowapokea tayari wanne wamepoteza maisha na wengine watatu wako 
katika hali mbaya na wamelazwa katika chumba cha wagonjwa wa dharura,” 
alisema Dk. Samky.
  Aidha alisema  majeruhi wengine 16 wanaendelea kupata matibabu 
hospitalini hapo kwa kuchukuliwa vipimo wakati watakaokuwa wamepata 
matibabu wataruhusiwa kwenda nyumbani.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa ajali hiyo, ilitokea majira ya saa nane 
kasoro robo mchana ambapo roli likiwa katika mwendo kasi likijaribu 
kukata kona kali lilizidiwa hivyo tela kuigonga Costa na kusababisha 
ajali hiyo.
  Akizungumza katika eneo la tukio Safari Samson shuhuda wa ajali hiyo 
aliwaambia waandishi wa habari kuwa dereva wa Costa aliyemtambua kwa 
jina moja la Mwasa mkazi wa Ilomba jijini Mbeya ni mmoja wa watu 
waliofariki papo hapo.
“Nimefika eneo hili mapema sana kwani Costa hii ni ya ndugu yangu 
baada ya kupigiwa simu kuwa gari ya ndugu yangu imepata ajili, 
nilishuhudia maiti nane ikiwamo ya dereva wa Costa zikitolewa eneo hili 
na kwenye roli tumetoa maiti moja ambapo dereva wa roli amekimbia,” 
alisema.
  Naye utingo wa roli lililopata ajali, Christopher Mgaya (32), mkazi wa
 Dar es Salaam alisema kuwa walikuwa wakitokea mpakani kuelekea Dar es 
Salaam wakishuka katika mtelemko kwenye kona aliona Costa ikipandisha 
mlima ghafla tela lilicheza ndipo mwenye Costa akajibamiza kwenye tela 
na kusababisha ajali hiyo.
  “Kwenye roli tulikuwa watatu, mimi, dereva ninayemtambua kwa jina moja
 tu la Peter pamoja na abiria mmoja ambaye tulimpakia akiwa na mzigo 
wake wa maparachichi na machungwa hata hivyo alifariki, lakini dereva 
amenieleza kuwa shingo inamuuma sana hivyo ametangulia hospitali.
No comments:
Post a Comment